IQNA

Saudia iuuombe radhi Umma wa Kiislamu kufuatia maafa ya Mina

16:17 - September 27, 2015
Habari ID: 3372415
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema Ulimwengu wa Kiislamu una maswali mengi ya kuuliza kuhusu maafa yaliyotokea Mina nchini Saudi Arabia.

Akizungumza mapema leo Jumapili mjini Tehran mwanzoni mwa darsa yake ya fiqhi  ya "Kharij"  (darsa ya daraja la juu kabisa la fiqhi), Ayatullahil Udhma Sayyid Ali Khamenei aliongeza kwamba watawala wa nchi hiyo wanapaswa kuuomba radhi Umma wa Kiislamu na familia zilizopatwa na msiba badala ya kuzituhumu pande nyingine; vilevile watalawa wa Saudia wanapaswa kukubali jukumu na kuhusika kwao na maafa hayo makubwa na kushughulikia taathira zake.
Ayatullah Khamenei ameashiria tukio la kusikitisha la vifo vya mahujaji katika eneo la Mina lililoifanya sikukuu ya Idul Adh’ha kuwa msiba kwa Umma wa Kiislamu na kusema: Mwanadamu yeyote hawezi kuondokewa na huzuni na ghamu kubwa ya tukio hilo na huzuni hiyo inazilemea nyoyo zetu na Waislamu wote katika siku hizi.
Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema hatua ya watawala wa Saudi Arabia ya kuzilaumu pande nyingine na kutaka kujivua na jukumu la kuhusika ya maafa hayo si sahihi na ni hatua butu na isiyo na tija. Ameongeza kuwa: Ulimwengu wa Kiislamu una maswali mengi ya kuuliza kwani kufariki dunia zaidi ya watu elfu moja katika tukio hilo si jambo dogo; kwa msingi huo ulimwengu wa Kiislamu unapaswa kutafakari kuhusu suala hilo.
Amesisitiza kuwa kadhia hii haitasahaulika na mataifa mbalimbali yataifuatilia ipasavyo, hivyo Wasaudia- badala ya kuzitupia lawama na kuzituhumu pande nyingine-, wanapaswa kubeba dhima na masuulia ya kuhusika na maafa hayo.../mh

3370995

captcha