Tarehe 22 Bahman, Hijria Shamsia inayosadifiana na Februari 11 kila
mwaka, huwa ni siku ya kufikia kileleni sherehe za ushindi wa Mapinduzi
ya Kiislamu ya Iran. Tarehe 11 Februari 1979, sawa na tarehe 22 Bahman
mwaka 1357 Hijiria Shamsia, Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran yakiongozwa na
Imam Khomein (MA) mwasisi mkuu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran
yalifanikiwa kuupindua utawala kibaraka wa Kipahlavi. Katika maadhimisho
ya leo, mamilioni ya wananchi waliokuwa wameshika picha za Imam
Ruhullah Khomeini (MA) na Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah
Sayyid Ali Khamenei, wametoa nara za 'Kifo kwa Marekani' 'Kifo kwa
Israel' 'Kifo kwa utawala wa Aal Saud' na 'Labbaika yaa Khamenei', na
kwa mara nyingine wametangaza utiifu wao kwa malengo matukufu ya
Mapinduzi ya Kiislamu na kwa Imam Khomeini, Mwasisi wa Jamhuri ya
Kiislamu ya Iran. Zaidi ya wandishi wa habari 5200 wa ndani na nje ya
Iran walikuwepo kuripoti maadhimisho ya leo hapa nchini. Aidha zaidi ya
wageni 450 kutoka nchi 28 wakiwemo shakhsia wa kielimu, kisiasa na
viongozi wa ngazi za juu wa nchi za Ulaya, Afrika, Asia na Marekani,
walihudhuria katika shere hizo ambazo zimefana sana. Baada ya maandamano
ya kuadhimisha Mapinduzi ya Kiislamu, waandamanaji wamesoma azimio lao
la siku ya Mwenyezi Mungu ya 22 Bahman hapa mjini Tehran. Katika azimio
hilo, waandamanaji wameyataja mafanikio na uwezo wa Iran ya Kiislamu
katika sekta ya ulinzi hususan uwezo wa makombora, kuwa ni mambo ambayo
ni haki ya wazi ya Iran na hayafai hata kujadiliwa. Aidha wameyaonya
madola ya kibeberu kuwa endapo yatajaribu kuidhoofisha au kuitisha Iran,
basi taifa la Iran kwa msaada wa vikosi vyake vya ulinzi litatoa
majibu makali mno kwa aui atakaeleta chokochoko zozote zile.
Katika maadhimisho hayo Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya
Iran, amehutubia umati mkubwa uliokusanyika kwenye uwanja wa Azadi hapa
Tehran na sambamba na kuashiria kupanuliwa wigo wa makubaliano baina ya
Iran na Russia, China na Umoja wa Ulaya kwa ajili ya kuwa na ushirikiano
wa pamoja wa muda mrefu, amesema kuwa, dunia ya leo imetambua kuwa,
kipindi cha kutumia lugha ya vikwazo na kulivunjia heshima taifa la Iran
kimepita na kwamba sasa umewadia wakati wa kuzungumza na Iran ya
Kiislamu kwa lugha ya heshima na busara. Katika sehemu nyingine ya
hotuba yake, Rais Rouhani amesema kuwa, Wairani ni watu wa amani na
usalama katika eneo hili na dunia nzima kwa ujumla.
3474869