IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi:

Wafanyabiashara wa Uswisi wawekeze Iran na kuboresha biashara ya pande mbili

11:17 - February 28, 2016
Habari ID: 3470167
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Jumapili alifanya mazungumzo na Rais Jwa Uswisi aliyekuwa safarini Iran.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Ali Khamenei katika mazungumzo hayo na Rais Johann Schneider-Ammann wa Uswisi aliashiria historia ya uhusiano wa nchi hizo mbili na taswira nzuri ya mwenendo wa Uswisi katika fikra za Wairani na amekaribisha suala la kuzidishwa ushirikiano wa kiuchumi na kielimu wa pande mbili. Amesema kiwango cha mabadilishano ya kibiashara kati ya Iran na Uswisi ni kidogo na hakina mlingano, na kusisitiza kwamba, wafanyabiashara na wawekezaji wa Uswisi wanaweza kuboresha mizani hiyo kwa kuelewa vyema uwezo mkubwa wa Iran.
Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema historia ya Uswisi ya kutojiunga na mashinikizo na vikwazo vya baadhi ya nchi za Magharibi dhidi ya Iran ni miongoni mwa nyanja nzuri za kiutamaduni kwa ajili ya kuzidisha ushirikiano wa pande hizo mbili. Ameongeza kuwa: "Tangu awali sisi tunaitambua Uswisi kuwa ni kituo cha amani, urafiki na ushirikiano lakini baadhi ya nchi za Ulaya hazina sifa hizo na zinayaona maslahi yao katika kuanzisha vita na kochochea hitilafu”.
"Tunaitambua Uswisi kuwa ni kituo cha amani, urafiki na ushirikiano lakini baadhi ya nchi za Ulaya hazina sifa hizo na zinayaona maslahi yao katika kuanzisha vita na kochochea hitilafu”.
Ameashiria pia tajiriba ya wananchi wa Iran kuhusu hatua ya baadhi ya nchi za Ulaya ya kuchochea vita ikiwa ni pamoja na kuupatia utawala wa Saddam Hussein makombora na ndege za kivita wakati wa vita vilivyoanzishwa na utawala huo dhidi ya Iran na akasema: Mwenendo huo umejenga taswira hasi katika fikra za wananchi wa Iran lakini taswira kama hiyo haiko hapa nchini kuhusu Uswisi.
Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa, serikali ya Jamhuri ya Kiislamu inaunga mkono kikamilifu mahusiano ya kiuchumi na dhamana ya kisheria ya makubaliano ya Iran na Uswisi na kuongeza kuwa, jambo muhimu ni kuona makubaliano hayo yakitekelezwa kivitendo kwa ushirikiano halisi, azma na irada thabiti.
Katika mkutano huo ambao pia umehudhuriwa na Rais Hassan Rouhani, Rais Johann Schneider-Ammann wa Uswisi ameeleza kufurahishwa kwake na safari yake hapa nchini na kuashiria historia ya miaka mingi ya uhusiano wa kirafiki wa nchi yake na Iran. Amesema: "Ni fahari kwetu sisi kuwa hapa Iran na tunashuhudia harakati inayosonga mbele ya uhusiano wa nchi hizi mbili”.
Bwana Johann Schneider-Ammann amesema kuwa anaandamana na ujumbe mbili za kielimu na kiuchumi hapa nchini na kuongeza kuwa, katika safari yake mjini Tehran kumejadiliwa ramani ya njia ya ushirikiano mpana zaidi na wa nyanja mbalimbali kati ya Iran na Uswsi na kwamba, kutiwa saini ramani hiyo ya njia kunaweza kupeleka kupanuliwa zaidi uhusiano wa pande mbili.
Rais wa Uswisi amegusia pia changamoto kubwa zilizopo duniani na kusema: Athari za mtikisiko na changamoto hizo zimefika hata Ulaya na kandokando ya Uswisi na kunahitaji ushirikiano kwa ajili ya kukabiliana na changamoto hizo.

3478804

captcha