Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, maonyesho hayo ya siku mbili yanatazamiwa kuanza tarehe 19 Novemba katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Kenyatta, KICC, jijini Nairobi. Inatazamiwa kuwa kutakuwa na vibanda 300 vya wafanyabiashara wa kitaifa na kimataifa ambao wataonyesha bidhaa na huduma zao halali. Maonyesho hayo ni ishara ya kuongezeka Waislamu ambao wanataka bidhaa na huduma ambazo zinaenda sambamba na mafundisho ya dini ya Kiislamu.
Kinyume na inavyodahniwa na wengi, nembo ya 'Halal' haitumiki tu kaatika chakula na hasa nyama, bali pia huduma kama vile za benki na bima.
Mmoja wa maafisa wa habari katika maonyehso hayo, Miswaleh Zingizi wa Shirika la Mawasiliano la Kijani ameliambia gazeti la Standard la nchini Kenya kuwa, mbali na kustawisha biashara, maonyesho hayo pia yanalenga kuondoa dhana zisizo sahihi kuhusiana na utumizi wa bidhaa na huduma maarufu kama 'Halal' katika jamii. Ameongeza kuwa, "Katika hali ambayo wengi hudhani istilahi ya 'Halal' inahusu vyakula tu, ukweli ni kuwa ' Halal' pia inahusu sekta kama vile uwekezaji, huduma za benki, bima, usafiri, dawa, utalii, vipodozi, ununuzi na uuzaji nyumba n.k.
Maonyesho ya Halal Kenya yatakuwa ni jukwaa la kubadilishana habari, wafanya biashara kujuana na pia wananchi kujifunza mengi kuhusu fursa na huduma za sekta ya Halal.
Kwa mujibu wa takwimu, sekta ya 'Halal' duniani sasa ina thamani ya $2.1 Trilioni (Ksh Bilioni 210) na ni kati ya sekta zinazostawi kwa kasi duniani.
Mwaka 2008, Kenya ilikumbatia mfumo wa kifedha wa Kiislamu na hivyo kupelekea kufunguliwa benki kadhaa ambazo zinaendeshwa kwa mujibu wa Sharia za Kiislamu. Aidha mashirika kadhaa yamefungua mfumo wa bima ya Kiislamu (takaful) huku kukiwa na jitihada za uwekezaji wa Kiislamu katika soko la hisa.
Kutokana na
idadi kubwa ya Waislamu nchini Kenya na Afrika ambao wanataka kuendesha maisha
yao kwa mujibu wa mafundisho ya Kiislamu, kuna fursa kubwa ya bidhaa na huduma
halali kote Afrika.