Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Mohammad Javad Zarif amemuandikia barua katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akitaka umoja huo uzingatie zaidi hali mbaya ya Waislamu wa kabila la Rohingya wanaoteswa na kuangamizwa nchini Myanmar.
Katika barua yake hiyo, Zarif amebainisha wasiwasi wake kuhusu hali mbaya ya Waislamu wa kabila la Rohingya na kuongeza kuwa: "Serikali ya Myanmar inapaswa kufahamishwa udharura wa kusitisha mara moja ukiukwaji wa haki za Waislamu sambamba na kuhakikisha wanapata misaada ya haraka ya kibinadamu."
Katika barua hiyo kwa Guterres, Zarif ameongeza kuwa: "Waislamu Warohingya mbali na kuwa wamepokonywa haki yao ya kimsingi ya kuwa wenyeji wa ardhi yao, kila siku wanakabiliwa na mauaji na mateso huku idadi kubwa miongoni mwao wakiwa wakimbizi katika nchi zingine."
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran katika barua yake ameongeza kuwa, hali ya Waislamu Warohingya ni kinyume kabisa na hati ya Umoja wa Mataifa na mikataba ya kimsingi ya haki za binadamu. Amesema hali ya kusikitisha ya Waislamu hao ni jambo ambalo limewatia wasi wasi mkubwa Waislamu duniani. Waziri Zarif amesema kuvunjiwa haki za kimsingi Waislamu Warohingya ni jambo linaloweza kuvuruga uthabiti na usalama nchini humo na pia katika nchi jirani.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ameseama anataraji jamii ya kimatiafa na serikali ya Myanmar itachukua hatua ili kuzuia Mabudha wenye misimamo mikali kuwakandamiza Waislamu.
Hivi karibuni John McKissick, Mkuu wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR kusini mwa Bangladesh ametangaza kuwa, jeshi la Myanmar na viongozi wa serikali ya nchi hiyo wamekuwa wakiwalazimisha Waislamu wa jamii ya Rohingya kuyahama makazi yao na kukimbilia katika nchi jirani. Afisa huyo wa Umoja wa Mataifa amesisitiza kuwa serikali ya Myanmar inatekeleza mauaji ya kimbari dhidi ya Waislamu.
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa Waislamu wa kabila la Rohingya ni jamii ya wachache duniani inayodhulumiwa na kunyongeshwa zaidi. Serikali ya Myanmar inakataa kuwapa haki za uraia Waislamu hao ambao idadi yao ni zaidi ya watu milioni moja na laki tatu.
Katika miaka ya karibuni, Waislamu wengi wa kabila la Rohingya nchini Myamnar wameuawa au kulazimika kuhama makazi yao na kuwa wakimbizi katika nchi za Thailand, Malaysia na Indonesia kutokana na mashambulio ya vikosi vya serikali na Mabudha wenye misimamo ya kufurutu mpaka wanaoungwa mkono na serikali ya nchi hiyo.