Akizungumza na IQNA, katibu wa kongamano hilo Hujjatul Islam Sayyed Mohammad Naqib amesema Makala 16 zitawasilishwa katika kikao hicho cha siku moja cha wataalamu wa ngazi za juu.
Ameongeza kuwa, kongamano hilo litafanyika katika Chuo cha Kidini cha Imam Kadhim AS mjini Qum ambapo kutakuwa na vitengo viwili. Hujjatul Islam Naqib amesema wasomi 20 wa kigeni ni kati ya wageni waalikwa katika mkutano huo.
Wasomi watakaowakilisha Makala katika mkutano huo ni kutoka Iran, Malaysia, Syria, Australia, Russia, Italia, Zimbabwe, Marekani, India na Lebanon. Amesema Makala zilizochaguliwa kuwasilishwa katika kongamano hilo zimechaguliwa kutoka makala 421 za wasomi kutoka maeneo mbali mbali duniani.
Kwa muda wa miaka 10 sasa kongamano la kimataifa la masomo ya Qur’ani limekuwa likifanyika pembizoni mwa mashindano ya kimataifa ya Qur’ani Tukufu.
Mashindano ya 34 ya Kimataifa ya Qur’ani Tukufu ya Iran yalifunguliwa rasmi Jumatano Aprili 19 na yataendelea kwa muda wa siku sita hapa Tehran, hadi tarehe 27 Rajab, katika Ukumbi wa Sala wa Imam Khomeini MA ambapo kuna washiriki 276 kutoka nchi 83 duniani.