Katika taarifa, OIC imebainisha masikitiko yake kuhusu mauaji hayo yaliyojiri baina ya 12 na 13 mwezi huu wa Mei katika mji wa Bangassou ambapo Waislamu karibu 30 waliuawa. Aidha katika mauaji hayo askari wanne kulinda amani wa Umoja wa Mataifa pia waliuawa.
Katibu Mkuu wa OIC Dkt. Yousef Al Al-Othaimeen ametuma salamu zake za rambi rambi kwa familia za waliopoteza maisha katika hujuma hiyo. Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa sambamba na kulaani mauaji hayo, limewataka viongozi wa Jamhuri ya Afrika ya Kati kuanzisha uchunguzi mara moja dhidi ya waliotekeleza shambulio hilo,na kuitaka serikali ya Bangui kufanya uchunguzi kuhusiana na askari waliotoweka wa kikosi hichocha Umoja wa Mataifa.