Taarifa zinasema waandamanaji wametoa nara za kuulani utawala wa ukoo wa Aal Khalifa ambao unaendelea kutumia mkono wa chumo kukandamiza maandamano ya amani.
Waandamanaji katika Siku ya Idul Adha wamalaani vikali hatua ya utawala kuendelea kuwashikilia korokoroni wafungwa wa kisiasa, hasa wanawake, na kutaka waachiliwe huru mara moja.
Hayo yanajiri wakati ambao mzingiro uliowekwa na askari wa utawala wa Aal Khalifa katika eneo la Ad-Diraz yalipo makaazi ya Sheikh Isa Qassim, kiongozi wa kimaanawi wa mapinduzi ya wananchi wa Bahrain ulitimiza siku mia moja Septemba Pili.
Kwa mnasaba wa kutimia siku mia moja hii leo tangu kuwekwa mzingiro huo katika eneo ilipo nyumba ya Sheikh Isa Qassim, wanaharakati wa Bahrain wameweka picha mbalimbali kwenye mitandao ya kijamii zinazoonyesha magari mawili ya deraya katika eneo la Ad-Diraz na kutoa taswira halisi ya hali inayotawala katika eneo hilo.
Kabla ya hapo, kwa kutumia mashtaka bandia, utawala wa kiimla wa ukoo wa Aal Khalifa ulimvua uraia Sheikh Isa Qassim. Baadhi ya wanaharakati wa kisiasa nchini Bahrain wanaitakidi kuwa utawala wa Manama umechukua hatua hiyo kwa madhumuni ya kumuondoa nchini humo na kumbaidisha kiongozi huyo wa vuguvugu la mapinduzi ya wananchi wa Bahrain.
Tangu mwezi Februari 2011 hadi sasa, Bahrain inaendelea kushuhudia wimbi la malalamiko ya wananchi wanaotaka mageuzi ya kisiasa, kuweko utawala wa sheria, kufanyika uchaguzi huru na wa kidemokrasia na kuondolewa ubaguzi na upendeleo wa kimadhehebu na kikaumu nchini humo.