IQNA

MSF yalaani hatua ya Saudia kushambulia kituo cha matibabu Yemen

10:10 - June 13, 2018
Habari ID: 3471555
TEHRAN (IQNA)- Shirika la Madaktari Wasio na Mipaka (MSF) limelaani hatua ya ndege za kivita za Saudi Arabia kudondosha mabomu katika kituo kimoja cha afya cha kuwatibu watu wenye kipindupindu nchini Yemen ambacho kinasimamiwa na shirika hilo.

Kufuatia hujuma hiyo ya Jumatatu uharibifu mkubwa umeripotiwa katika kituo hicho cha tiba katika mji wa Abs kaskazini magharibi mwa Yemen katika mkoa wa Hajjah na MSF imesema imesitisha kwa muda huduma zake katika eneo hilo.

Katika taarifa, mkuu wa MSF nchini Yemen amesema hujuma hiyo ya Jumatatu asubuhi dhidi ya kituo cha MSF cha kutibu kipindupindu, ilitekelezwa na muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudia pamoja na Imarati na ni ishara ya kutoheshimu vituo vya tiba na wagonjwa. 

MSF imesema inasitisha huduma zake huko Abs hadi pale itakapopata dhamana ya usalama wa wafanyakazi wake na wagonjwa. Wakuu wa MSF wanasema Saudia ilikuwa imefahamishwa eneo hilo ni la kutoa matibabu lakini imeamua kudondosha mabomu katika kituo hicho cha matibabu, jambo ambalo linahesabiwa kuwa jinai ya kivita.

Tangu mwezi Machi mwaka 2015, Saudia, ikisaidiwa na kuungwa mkono na baadhi ya nchi za Kiarabu hasa UAE na Marekani ilianzisha mashambulio ya kinyama dhidi ya Yemen kwa lengo la kutaka kumrejesha madarakani kibaraka wake Abd Rabbuh Mansur Hadi, rais wa nchi hiyo aliyejiuzulu na kuitoroka nchi.

Raia zaidi ya 14,000 wa Yemen wameuawa, hasa wanawake na watoto, na maelfu ya wengine kujeruhiwa katika uvamizi huo wa kijeshi huku Umoja wa Mataifa ukishindwa kuchukua hatua yoyote ya kuzuia jinai hizo za Saudia huko Yemen. Aidha watu zaidi ya laki sita wameambukizwa ugonjwa wa kipindupindu kote Yemen huku wengine zaidi ya 2,000 wakifarikia dunia tokea mwezi Aprili mwaka huu.

Halikadhalika kutokana na hujuma hiyo ya Saudia na UAE dhidi ya Yemen, Umoja wa Mataifa unasema watu milioni 20 kati ya jamii ya watu milioni 25 ya Yemen wanahitajia misaada ya kibinadamu.

3466054

captcha