Ayatullah Ahmad Jannati amesema hayo leo katika kikao cha Jopo la Wanazuoni Wanaomchagua Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ambapo ameashiria mashambulio ya mabomu ya Saudia katika sherehe ya harusi huko Yemen na kusema kuwa, kukaririwa kwa jinai hizo dhidi ya wananchi wasio na ulinzi, wanaokabiliwa na njaa na madhulumu wa Yemen kunafanyika chini ya kimya kizito cha wale wanaodai kuwa ni watetezi wa haki za binadamu.
Katibu wa Baraza la Kulinda Katiba ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuwa, utawala unaotenda jinai wa Saudia umekuwa ukiwalenga kwa makusudi raia wa Yemen na kumwaga kiholela damu zao.
Ayatullah Jannati ameashiria pia tukio chungu na la maafa la kutunguliwa na makombora ya Marekani ndege ya abiria ya Iran na kusisitiza kwamba, kuna haja ya kuwaonyesha walimwengu sura halisi ya haki za binadamu za Kimarekani.
Itakumbukwa kuwa, Julai 3, ilisaidifiana na tukio chungu la kutunguliwa ndege ya abiria aina ya Airbus ya Iran iliyokuwa ikitoka Bandar Abbas kusini mwa Iran kuelekea Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu. Manowari ya kijeshi ya Marekani USS Vincennes ilifyatua makombora mawili na kuua shahidi abiria wote 298 waliokuwa katika ndege hiyo. Shambulio hilo lilidhihirisha zaidi unyama wa serikali ya Marekani.