Fawzi Barhumi, msemaji wa Hamas ameitaja hatua ya Israel ya kufunga kivuko muhimu cha Kerem Shalom kuwa jinai dhidi ya Wapalestina, huku akiuonya vikali utawala huo juu ya matokeo mabaya ya kitendo chake hicho.
Kufungwa kwa kivuko hicho katika mji wa Rafah kutazuia kuingizwa katika eneo la Ghaza bidhaa za msingi zikiwemo za fueli, dawa na vifaa vya ujenzi.
Hata hivyo Waziri wa Vita wa Israel, Avigdor Lieberman amedai kuwa, njia hiyo muhimu itafungwa kuanzia leo Jumanne hadi Jumapili ijayo ili kuzuia kuingizwa mafuta na gesi pekee katika ukanda huo, na kuwa eti chakula na dawa zitaruhusiwa.
Lieberman amesema utawala huo haramu umechukua hatua hiyo ili kujibu kile anachodai kuwa ni 'njama za kigaidi' za Hamas.
Tokea mwaka 2007, utawala haramu wa Israel uliweka mzingira wa anga, nchi kavu na baharini dhidi ya Ukanda wa Ghaza baada ya Wapalestina katika eneo hilo kuichagua kidemokrasia harakati ya Hamas kuongeza eneo hilo. Mzingiro huo umelifanya eneo hilo lenye watu karibu milioni moja na nusu kutajwa kuwa gereza kubwa zaidi la wazi duniani.
Mbali na mzingiro huo, utawala haramu wa Israel pia umeanzisha vita mara tatu dhidi ya Ghaza tokea mwaka 2008 ambapo maelfu ya Wapalestina wakiwemo wanawake na watoto wameuawa.