IQNA

Sheikh Mkuu wa Al Azhar akosolewa kwa kupinga ndoa ya wake wengi

20:51 - March 05, 2019
Habari ID: 3471863
TEHRAN (IQNA)- Sheikh Mkuu wa Al-Azhar wa Al Azhar amekosolewa na wanazuoni wenzake wa Kiislamu nchini Misri kwa kudai kuwa "ndoa ya wake wengi ni dhulma kwa wanawake na watoto".

Katika matamshi yake Ijumaa iliyopita, Sheikh Ahmed al-Tayeb, Sheikh Mkuu wa Al Azhar nchini Misri alisema kuwa Waislamu wamefasiri visivyo aya za Qur'ani Tukufu kuhusu  suala la mume kuoa zaidi ya mke mmoja. Sheikh al-Tayeb amesema Qur'ani haijatoa idhini jumla ya kuoa wake wengi na kwamba, Qur'ani Tukufu imeruhusu ndoa hiyo katika baadhi ya hali tu.

Sheikh Mkuu wa Al Azhar ameashiria sehemu ya  aya ya 3 ya Surat An Nisa ya Qur'ani isemayo: "…  basi oeni mnao wapenda katika wanawake, wawili au watatu au wane. na mkiogopa kuwa hamwezi kufanya uadilifu, basi mmoja tu..." Akifafanua kuhusu aya hiyo Sheikh Ahmed al-Tayeb amesema katika hali ya sasa, ndoa ya wake wengi aghalabu huwa imeandamana na ujahili na kutofahamu Qur'ani Tukufu na Sunna ya Mtume Muhammad SAW.

Amedai katika aghalabu ya ndoa hizo wanawake na watoto hudhulumiwa. Amesema "wanawake ni nusu ya watu wote katika jamii na iwapo hatutawalinda itakuwa sawa na kutembea kwa mguu mmoja."

Lakini kauli hiyo ya Sheikh Ahmed al-Tayeb imepingwa vikali na wanazuoni wa Kiislamu nchini Misri na kuibua mjadala mkubwa nchini humo na kwingineko.

Sheikh Sameh Hamouda, imamu katika mji wa Alexandria amepinga kauli hiyo ya Sheikh Mkuu wa Al Azhar na kusema ndoa ya wake wengi ni dharura katika hali ya sasa ili kuwasitiri wanawake wengi Waislamu ambao wanakabiliwa na hatari  ya kuishi maisha yao yote pasina kuolewa. Sheikh Sameh Hamouda ameendelea kusema: "Ndoa ya wake wengi ni suluhiso kwa tatizo la idadi kubwa ya wanawake ambao bado hawajaolewa."

Jumamosi wiki hii, Al-Azhar imefafanua kuwa, kauli ya Sheikh al-Tayeb haimaanishi kuwa anaunga mkono marufuku ndoa ya wake wengi.

3468052

Habari zinazohusiana
captcha