IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Njama za Marekani dhidi ya Iran katika kadhia ya mafuta hazitabakia bila jibu

12:28 - April 25, 2019
Habari ID: 3471929
TEHRAN (IQNA)-Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa: "Katika kulipigisha magoti taifa la Iran, adui amejikita katika mashinikizo ya kiuchumi lakini afahamu kuwa, taifa hili katu halitapigishwa magoti na sambamba na kutumia vikwazo kama fursa ya kustawi na kunawiri, halitaacha uhasama wa Marekani ubakie hivi hivi bila kupata jibu."

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameyasema hayo Jumatano mjini Tehran wakati alipokutana na maelefu ya wafanyakazi wa sekta mbali mbali katika mwanzo wa 'Wiki ya Kazi na Mfanyakazi' nchini Iran.

Kiongozi Muadhamu ameashiria jitihada za Marekani za kuzuia uuzaji wa mafuta ghafi ya petroli ya Iran katika soko la kimataifa na kusema: "Taifa lenye harakati la Iran na viongozi waliomacho nchini Iran wameonyesha kuwa, iwapo watakuwa na hima, basi wanaweza kuvuka vizingiti na bila shaka jitihada hizo za Marekani zitaambulia patupu na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran itaweza kuuza kiasi chochote cha mafuta inachotaka katika soko la kimataifa."

Ayatullah Khamenei amekumbusha kuhusu nukta muhimu na kuwahutubu maadui wa taifa la Iran kwa kusema: "Mfahamu kuwa uadui wenu hautabaki bila jibu na taifa la Iran si taifa ambalo mtapanga njama dhidi yake na likae tu kama mtazamaji."

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria nukta nyingine kuhusu kushadidi mashinikizo ya mafuta ya Marekani dhidi ya Iran na kusema: "Kupunguza utegemezji wa pato la uuzaji mafuta kunapaswa kutazamwa kama fursa na hivyo tutumie fursa hiyo kutegemea zaidi uwezo wetu wa ndani ya nchi."

Ayatullah Khamenei aidha ameashiria madai ya wakuu wa Marekani na utawala wa Kizayuni na kusema: "Wao wanasema kuwa ni maadui wa mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu na kwamba eti si maadui wa wananchi wa Iran lakini kuhasimiana na Jamhuri ya Kiislamu ni kuhasimiana na taifa la Iran kwani Jamhuri ya Kiislamu imeasisiwa kwa msaada wa wananchi na iwapo wananchi hawangetoa msaada wao huo basi Jamhuri ya Kiislamu haingekuwepo."

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amebaini kuwa, kama ambavyo imesemwa hivi  karibuni, maadui sasa wako katika pumzi zao za mwisho kwani hatimaye watachoshwa na uhasama wao dhidi ya taifa la Iran lakini taifa hili halitachoka katika jitihada na mchakato endelevu wa ustawi."

3806125

captcha