IQNA

Magaidi waua watu 60 katika hujuma msikitini, sokoni nchini Nigeria

19:50 - May 02, 2018
Habari ID: 3471491
TEHRAN- (IQNA)- Watu zaidi ya 60 wameuawa katika hujuma mbili za kigaidi zilizolenga msikiti na soko kaskazini mashariki mwa Nigeria.

Taarifa zinasema katika hujuma hizo za Jumatano alasiri, mlipuko mmoja ulijiri katika msikiti mmoja huku wa pili ukitokea katika soko lililo karibu na msikito huo uliolengwa katika mji wa Mubi yapata kilomita 200 kutoka jimbo la Adamawa. Taarifa zaidi kutoka Nigeria zinasema kuwa, milipuko hiyo ya mabomu imetekelezwa na vijana wadogo ambao wanasadikiwa kuwa wafuasi wa kundi la magaidi wakufurishahi wa Boko Haram.

Baadhi ya duru za hospitali zinasema kuwa, idadi ya majeruhi wa milipuko hiyo ni kubwa na kwamba, hali ya baadhi yao ni mbaya. Baadhi ya majeruhi wamepelekwa katika hospitali ya Yola.

Milipuko hiyo ya mabomu imetokea siku chache tu baada ya kutokea mlipuko mwingine uliotekelezwa na kundi la kigaidi la Boko Haram huko Maiduguri.

Neno Boko Haram kwa ya lugha ya Kihausa lina maana ya 'elimu kutoka nchi za Magharibi ni haramu'. Zaidi ya watu elfu 20 wamepoteza maisha nchini Nigeria tokea kundi la Boko Haram lianzishe uasi mwaka 2009 huku wengine zaidi ya milioni mbili wakilazimika kukimbia makazi yao kutokana na ugaidi wa Boko Haram ambao sasa umeenea katika nchi jirani kama vile Cameroon, Niger na Chad.

Boko Haram ni kundi lenye misimamo ya kufurutu mipaka nchini Nigeria ambalo kutokana na kuwa na ufahamu mbaya na potofu kuhusiana na Uislamu, limeitumbukiza nchi hiyo katika dimbwi la machafuko na mauaji sambamba na kuzusha hitilafu za kidini na kikabila nchini humo.

3465704

captcha