Baada ya hatua kadhaa zilizochukuliwa na utawala wa Kizayuni kwa lengo la kunyakua baadhi ya maeneo ya Ufukwe wa Magharibi wa Mto Jordan na kuyaambatisha na ardhi ulizozipa jina la 'Israel', Mahmoud Abbas ametangaza kuwa, Harakati ya Ukombozi wa Palestina (PLO) na Mamlaka ya Ndani ya Palestina hazitaheshimu tena wala kutekeleza makubaliano yoyote ziliyofikia na Tel Aviv na Washington.
Abbas amesema, Marekani ni mkosa kuhusiana na dhulma wanazofanyiwa wananchi wa Palestina na akafafanua kuwa,Washington ni mshirika wa Tel Aviv katika hatua zake za kighasibu.
Hivi karibuni viongozi wa utawala wa Kizayuni wa Israel walikubaliana kuwa ifikapo mwezi Julai mwaka huu, waanze kutekeleza mpango wa kuyaambatisha baadhi ya maeneo ya eneo la Ufukwe wa Magharibi wa Mto Jordan na ardhi zingine za Palestina unazozikalia kwa mabavu.
Makadirio yaliyofanywa yanaonyesha kuwa, unyang'anyi na uambatishaji huo utajumuisha zaidi ya asilimia 30 ya eneo la Wapalestina la Ufukwe wa Magharibi.