IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Marekani na washirika wake wanalisaidia kundi la kigaidi la ISIS

18:29 - November 23, 2015
Habari ID: 3456282
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Ali Khamenei kabla ya adhuhuri ya leo amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria aliyeko safarini hapa nchini.

Katika mazungumzo hayo Ayatullah Khamenei amesema kuwa, kuna udharura wa kuzidishwa ushirikiano baina ya nchi za Kiislamu katika kulinda utambulisho wa Uislamu na Waislamu. Amesisitiza kuwa, miungano ya kimataifa inayodai kupambana na mirengo ya kigaidi haiwezi kuaminiwa kwa njia yoyote ile kwa sababu waharibifu hao hususan Marekani ndio waanzilishi au waungaji mkono wa nyuma ya pazia wa makundi ya kigaidi kama lile la ISIS au Daesh.
Ayatullah Khamenei amesema kuwa, maadui wa waziwazi wa Uislamu na maadui mbao wanaifanyia uadui dini ya Uislamu kwa kutumia jina la Uislamu ni mithili na pande mbili za mkasi. Ameongeza kuwa, nchi za Kiislamu zinapaswa kulinda utambulisho na maslahi yao kwa kuzidisha ushirikiano ili kuweza kupambana na maadui hao hatari.
Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, ni makosa kuwa na matarajio ya ushirikiano na msaada wa Marekani na Magharibi katika kupambana na mirengo ya kigaidi kama Daesh na Boko Haram. Ameongeza kuwa, ripoti za kuaminika zinaonesha kwamba, Wamarekani na baadhi ya nchi zilizobakia nyuma za eneo hili wanalisaidia moja kwa moja kundi la Daesh nchini Iraq na kushiriki katika uharibifu.
Amesema kuwa kuzidishwa ushirikiano wa nchi za Kiislamu hakuna maana ya kufunga na kukata uhusiano na nchi nyingine na kuongeza kuwa, Jamhuri ya Kiislamu ina uhusiano mpana na nchi zote isipokuwa Marekani na utawala wa Kizayuni wa Israel lakini inaamini kuwa, nchi za Kiislamu zinapaswa kukaribiana zaidi.
Ayatullah Khamenei ameeleza kufurahishwa kwake na kuchaguliwa Bwana Buhari, ambaye ni Muislamu mwenye kushikama na dini, kuwa Rais wa nchi kubwa na muhimu ya Nigeria na akasema, kuna nyanja nyingi za kuweza kushirikiana kati ya nchi hizi mbili. Amesisitiza kuwa nyanja na uwezo huo unapaswa kutambuliwa na kutumiwa.
Kwa upande wake Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria amesema katika mazungumzo hayo ambayo pia yamehudhuriwa na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Iran kwamba uhusiano wa nchi yake na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni wa siku nyingi na imara. Amesema Iran ni nchi iliyoendelea, kubwa na yenye uwezo kwa ajili ya uhusiano na ushirikiano.
Rais wa Nigeria ameishukuru Iran kwa mwaliko wa kushiriki katika mkutano wa nchi zinazouza gesi kwa wingi duniani na kusema: "Hii leo katika mazungumzo yangu na Kiongozi Muadhamu nimejifunza mengi na ninathamini na kuenzi mazungumzo na miongozi niliyopata".

Kabla ya mazungumzo hayo Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu pia alikuwa amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Nicolas Maduro wa Venezuela ambako alisema kuwa Marekani inafanya njama za kutokomeza mapambano ya Venezuela dhidi ya Washington. Amepongeza kusimama kidete na harakati inayotoa ilhamu ya Venezuela katika kupambana na siasa za kibeberu na kusisitiza kuwa: Hii leo siasa za kibeberu zimekuwa balaa kubwa kwa maisha ya wanadamu na njia pekee ya maendeleo na ushindi kwa njia zinazojitawala ni kusimama imara na kutegemea nguvu ya wananchi katika vita vya irada na matakwa tofauti.
Amesema maendeleo ya kustaajabisha ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika nyanja za sayansi na teknolojia, licha ya mashinikizo makubwa na vikwazo vya maadui, ni uzoefu na tajiriba yenye thamani kubwa na ametilia mkazo udharura wa kuzidishwa kiwango cha ushirikiano wa nchi mbili za Iran na Venezuela.

3456070

captcha