Sambamba na kuwadia mwezi 17 Mfunguo Sita, siku ya kuadhimisha Maulidi
ya Bwana Mtume Muhammad SAW na Imam Jafar Sadiq AS, viongozi wa mfumo wa
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na wageni walioshiriki kwenye mkutano wa
Umoja wa wa Kiislamu, mabalozi wa nchi za Kiislamu na majimui ya
wananchi wa matabaka tofauti, leo asubuhi wameonana na Kiongozi Muadhamu
wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Ali Khamenei mjini Tehran.
Katika mkutano huo, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu sambamba
na kutoa mkono wa baraka na fanaka kwa mnasaba wa maadhimisho ya siku
ya kuzaliwa Bwana Mtume mtukufu SAW na Imam Sadiq AS ameashiria suala la
kupulizwa roho ya uhai na umaanawi wa kweli baada ya ujio wa Mtume wa
Uislamu na namna neema ya kuzaliwa Bwana Mtume Muhammad SAW na kudhihiri
Uislamu ilivyoweza kuhuisha dunia iliyokuwa imekufa na kuteketezwa na
ujahilia na kusema kuwa, jukumu kubwa zaidi la ulimwengu wa Kiislamu leo
hii hususan kwa maulamaa na wasomi wanaoangalia mambo kwa njia sahihi,
ni kufanya jitihada kubwa za dhati kwa ajili ya kupuliza roho ya kweli
ya Uislamu na masuala ya kiroho ulimwenguni dhidi ya dhulma, ubaguzi na
machafuko yaliyoenea kila mahali duniani leo. Amesisitiza kuwa, hivi
sasa ni zamu ya ulimwengu wa Kiislamu kutumia elimu na suhulka za kisasa
duniani na vile vile akili na hekima na tadibiri na mtazamo wa mbali
kwa ajili ya kusimamisha ustaarabu mpya wa Kiislamu duniani.
Ayatullah Khamenei amesema kuwa suala la kuadhimisha siku ya kuzaliwa
Mtume wa Uislamu SAW ni muhimu sana, lakini umuhimu wake ni mdogo mno
ikilinganishwa na umuhimu wa kutekeleza inavyopasa majukumu yanayotakiwa
hivi sasa katika ulimwengu wa Kiislamu na kuongeza kuwa: Majukumu ya
umma wa Kiislamu hayamalizikii tu kwenye kuadhimisha siku ya kuzaliwa
Bwana Mtume Muhammad SAW au siku ya kubaathiwa na kupewa kwake Utume,
bali ulimwengu wa Kiislamu unapaswa uelekeze zaidi nguvu zake katika
kuunda ustaarabu mpya wa Kiislamu.
Ameongeza kuwa: Ustaarabu mpya wa Kiislamu hauna maana ya kuvamia ardhi
za watu wengine, wala kukanyaga haki za binadamu na wala kuyatwisha
mataifa mengine akhlaki na utamaduni hu wa Kiislamu na vitu kama hiyo
ambavyo vinafanywa na ustaarabu wa Magharibi, bali ulimwengu wa Kiislamu
unapaswa hima yake yote iwe ni kufikia kwenye staarabu wake wa
Kiislamu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amegusia pia namna
Wamagharibi walivyotumia elimu na falsafa ya ulimwengu wa Kiislamu kwa
ajili ya kujenga ustaarabu wao na kuongeza kuwa: Ijapokuwa ustaarabu huo
wa Magharibi umeonesha mambo mazuri ya kiteknolojia, kasi ya maendeleo,
urahisi wa kufikia baadhi ya mambo na zana mbali mbali za kisasa za
maisha ya mwanadamu, lakini umeshindwa kumletea mwanadamu furaha,
ufanisi na uadilifu bali pia kunashuhudiwa migongano na mikinzano hata
ndani ya ustaarabu huo wenyewe wa Magharibi.
Ayatullah Khamenei ameongeza kuwa, katika dhahiri yake, ustaarabu wa
Magharibi unaonekana ni ustaarabu wenye mambo mengi mazuri na mvuto
mkubwa, lakini hivi sasa imethibitika kuwa katika upande wa maadili,
ustaarabu huo ni fasidi na mbovu kabisa na katika upande wa umaanawi pia
ni pumba na bua kiasi kwamba hata Wamagharibi wenyewe wanaukiri
waziwazi uhakika huo.
Aidha amesisitiza kuwa hivi sasa ni zamu ya ulimwengu wa Kiislamu
kuweka misingi madhubuti ya ustaaarabu mpya wa Kiislamu na kuongeza
kuwa: Wanasiasa wa ulimwengu wa Kiislamu si watu wa kutegemewa katika
jitihada za kulifikia lengo hilo na kwamba maulamaa wa kidini na wasomi
wa kweli ambao kibla chao si Magharibi, wanapaswa wafanye kazi ya
kuwaamsha watu katika umma wa Kiislamu na wajue kuwa, ni jambo
linalowezekana kabisa kuanzisha ustaarabu wa namna hiyo.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amegusia uwezo na nafasi
pana ya ulimwengu wa Kiislamu ikiwa ni pamoja na kuwa na ardhi nzuri
zilizoko kwenye maeneo bora kabisa ya kijiografia, utajiri mkubwa wa
maliasili na nguvu kazi yenye vipaji vya kila namna na kuongeza kuwa:
Iwapo uwezo huo ulio nao ulimwengu wa Kiislamu utaoanishwa vizuri na
mafundisho ya kweli ya Uislamu, basi umma wa Kiislamu utaweza kuonesha
kwa namna nzuri kabisa ubora wa vipaji vyake katika nyuga za kielimu na
kisiasa na kiteknolojia na vile vile katika nyanja za kijamii.
Ayatullah Khamenei ameutaja mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kuwa
ni mfano mzuri wa uwezekano wa kuyafikia malengo hayo makubwa na
kuongeza kuwa: Kabla ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Iran ilikuwa
imebaki nyuma sana katika upande wa kielimu, kisiasa na kijamii na
katika upande wa kisiasa ilikuwa imetengwa na katika upande wa masuala
ya ndani ya nchi pia ilikuwa ni tegemezi kikamilifu. Lakini leo hii kwa
baraka ya Uislamu, taifa la Iran limeonesha utambulisho na shakhsia yake
na nchi imepiga hatua kubwa muhimu za kielimu na kiteknolojia na elimu
za kisasa kiasi kwamba imekuwa ni moja ya nchi bora katika nyanja hizo
duniani.
Ayatullah Khamenei vile vile amesisitiza kuwa, mfano huu unaweza kuenea
na kushuhudiwa katika ulimwengu mzima wa Kiislamu na kuongeza kuwa:
Hata hivyo kufikia kwenye nafasi hiyo kuna masharti yake na miongoni mwa
masharti hayo ni kupunguzwa nguvu za jinamizi la madola ya kibeberu kwa
mataifa ya Waislamu suala ambalo tab'an lina gharama zake kwani ni
jambo lisiloyumkinika kufikia malengo makubwa kama hayo bila ya
kuyagharamikia.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa, katika
ustaarabu wa Kiislamu - tofauti na ustaarabu wa Magharibi - hakuna nchi
yoyote itakayokuwa chini ya ubeberu wa nchi nyingine. Ameongeza kuwa,
katika kuweka misingi ya ustaarabu mpya wa Kiislamu, hatupaswi kuelekeza
macho yetu kwa Wamagharibi na wala kutekwa na tabasamu au kuchukia
kwao, bali tunachopaswa kufanywa ni kuendelea na njia yetu sahihi kwa
kutegemea uwezo na suhula zetu wenyewe.
Ayatullah Khamenei amesema kuwa, moja ya mbinu zinazotumiwa na maadui
kwa ajili ya kuzuia kuundwa ustaarabu mpya wa Kiislamu, ni kuzusha
mifarakano na mizozo baina ya Waislamu. Ameongeza kuwa: Tangu suala la
Ushia na Usuni lilipoanza kuingizwa kwenye msamiati wa viongozi wa
kisiasa wa Marekani, watu wenye ufahamu na wenye muono wa mbali
walikumbwa na wasiwasi kwani ilionekana wazi kuwa, viongozi hao wa
Marekani wameanzisha njama mpya na hatari zaidi kuliko za huko nyuma
dhidi ya ulimwengu wa Kiislamu.
Amesisitiza kuwa, Wamarekani wanapinga asili ya Uislamu na hatupaswi
kudanganywa na matamshi yao ya kujifanya wanayaunga mkono baadhi ya
makundi ya Waislamu. Ameongeza kuwa: Matamshi ya rais wa zamani wa
Marekani baada ya kutokea matukio ya tarehe 11 Septemba ambaye
alitangaza wazi kuanza vita vya msalaba, kwa hakika ni uthibitisho
usiopingika wa kuweko vita vya ulimwengu wa kibeberu dhidi ya Uislamu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa matamshi
yanayotolewa na viongozi wa hivi sasa wa Marekani ya kudai wanakubaliana
na Uislamu, yanakwenda kinyume kabisa na uhalisia wa mambo.
Amesema: Viongozi wa hivi sasa wa Marekani wanapinga asili ya Uislamu
wenyewe; na tofauti na madai yao, wanachofanya ni kuzusha mifarakano
kati ya Waislamu, na mfano wa wazi wa jambo hilo, ni kuanzisha kwao
magenge ya kigaidi kama vile Daesh na magenge mengine ambayo yameundwa
na kusaidiwa kisilaha, kisiasa na kimafunzo kwa fedha za vibaraka wa
Marekani na ndio maana leo hii tunashuhudia maafa haya makubwa
yanayotokea katika ulimwengu wa Kiislamu hivi sasa.
Ayatullah Khamenei amesisitiza kwamba madai ya viongozi wa Marekani ya
kujifanya kuwa wanawaunga mkono Masuni kuliko Mashia ni uongo mkubwa na
kuongeza kuwa: Hivi kwani wananchi wa Ghaza ambao wanashambuliwa kwa
kila namna si Masuni? Je, wananchi wa Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan
(huko Palestina) ambao wako chini ya mashinikizo yote haya, si Masuni?
Vilevile amegusia matamshi ya mwanasiasa mmoja Mmarekani aliyesema
kuwa, adui wa Marekani ni fikra za Kiislamu na kusisitiza kwamba:
Wamarekani hawatofautishi baina ya Waislamu wa Kishia na Waislamu wa
Kisuni, bali wanampinga Muislamu yeyote yule anayeamua kuishi kwa mujibu
wa sheria na mafundisho ya Kiislamu na kusimama kidete kuupigania
Uislamu wake.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa, tatizo kuu
la Wamarekani dhidi ya Waislamu ni kushikamana kwao vilivyo na
mafundisho na sheria za Kiislamu na kufanya jitihada za kuanzisha
ustaarabu mpya wa Kiislamu.
Amesisitiza kuwa: Ni kwa sababu hiyo ndio maana wakati ulipoanza mwamko
wa Kiislamu, Wamarekani walishtushwa mno na mwamko huo na wakafanya
njama za kuudhibiti na wamefanikiwa kufanya hivyo katika baadhi ya nchi,
lakini mwamko wa Kiislamu si kitu kinachoweza kuzimwa na kwa uwezo wa
Mwenyezi Mungu mwamko huo utafikia tu malengo yake bila ya shaka yoyote
ile.
Ayatullah Udhma Khamenei amelitaja lengo na shabaha kuu ya kambi ya
kiistikbari kuwa ni kuzusha vita vya ndani vya baina ya Waislamu wenyewe
kwa wenyewe na kuangamiza miundombinu ya nchi za Waislamu kama vile
Syria, Yemen na Libya na kuongeza kuwa: Hatupaswi kunyamazia kimya na
kusalimu amri mbele ya njama hizo, bali tunapaswa kusimama imara
kukabiliana na njama hizo tukiwa tumejipamba kwa sifa za muono wa mbali
na kulinda istikama na kutotetereka.
Vilevile ameukosoa ulimwengu wa Kiislamu kwa kunyamazia kimya
mashinikizo waliyo nayo Waislamu wa Bahrain na mashambulizi ya usiku ya
mchana ya karibu mwaka mzima sasa wanayofanyiwa wananchi wa Yemen pamoja
na hali za Syria na Iraq, kama ambavyo ameashiria pia matukio ya hivi
karibuni ya nchini Nigeria na kusema kuwa: Kwa nini sheikh mpenda amani,
mrekebishaji wa umma, muumini na aliye tayari kuishi salama na watu
wote anafanyiwa ukatili wa kiasi chote hiki na karibu watu elfu moja
wanauliwa kiholela na wanawe wanauliwa shahidi na ulimwengu wa Kiislamu
unanyamaza kimya?
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza pia kuwa:
Malengo ya maadui wa Uislamu ni ya hatari sana na ni jukumu letu sote
kuwa macho na kuwa na muono wa mbali na kwamba ni jukumu la maulamaa wa
Kiislamu na wasomi wa kweli wa Kiislamu kuzungumza na wanasiasa wenye
mwamko na wenye uchungu na dini yao ili wayabainishe hadharani masuala
hayo.
Ayatullah Khamenei ameongeza kuwa: Katika hali ambayo ulimwengu
ulioghiriki katika matumizi ya mali na nguvu unatafuta njama hatari mno
za kuufanyia ulimwengu wa Kiislamu, hakuna mtu yeyote mwenye haki ya
kulala na kutoona mambo yanayotendeka dhidi ya Waislamu duniani leo.
Kabla ya hotuba ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Rais
Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ametoa mkono wa baraka kwa
mnasaba wa kukumbuka siku ya kuzaliwa Mtume mtukufu wa Uislamu SAW na
Imam Jafar Sadiq AS na kusema kuwa, Mtume wa Uislamu ni ruwaza njema ya
kimaadili na ucha Mungu na kuongeza kuwa: Bwana Mtume Muhammad SAW
amewaletea walimwengu somo la umoja, mshikamano, udugu na kupendana.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amebainisha kuwa, leo hii
tunahitajia mno kufuata mafundisho ya Bwana Mtume Muhammad SAW kuliko
wakati mwingine wowote na kusema kuwa: Kwa mshikamano wa taifa na
uongozi wa kiongozi wetu mtukufu, tumeweza kupata ushindi mbele ya
madola ya kibeberu na njia ya ushindi huo itaendelea.
Vile vile amezungumzia chaguzi mbili zinazokuja za Majlisi ya Ushauri
ya Kiislamu (Bunge la Iran) na ule wa Baraza la Wanavyuoni Wataalamu
(linalomchagua na kusimamia kazi za Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya
Kiislamu) na kusema kuwa chaguzi hizo ni mtihani wa kuonesha adhama na
haiba ya Iran kwa walimwengu na kuongeza kuwa: Kila mmoja anapaswa
kufikiria na kuupa kipaumbele ushindi wa mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu na
wa nchi katika chaguzi hizo.
Rais Rouhani ameashiria pia hamasa ya wananchi wa Iran ya tarehe 9 Dey
1388 (mwaka wa Kiirani wa Hijria Shamsia sawa na Disemba 30, 2009) na
kusisitiza kuwa, tarehe 9 Dey ni siku ya ulinzi wa taifa la Iran kwa
Ahlul Bait wa Bwana Mtume Muhammad SAW, kuulinda mfumo wa Jamhuri ya
Kiislamu, sheria na kulinda utawala wa fakihi na fakihi mtawala.
Rais Rouhani aidha amesema, usalama wa leo hii wa Jamhuri ya Kiislamu
ya Iran unatokana na busara, hekima, mipangilio mizuri na tadibiri ya
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu na ili kuweza kumshukuru
Mwenyezi Mungu kwa neema hiyo inabidi tuzidi kushikamana na kuusaidia
ulimwengu wa Kiislamu kwa ajili ya kuzikomboa nchi za ulimwengu huo
kutoka kwenye matatizo ya ugaidi na uingiliaji wa madola ya kibeberu
kwenye masuala ya ndani ya nchi hizo.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran aidha amebainisha kuwa, maadui
wameutumbukiza ulimwengu wa Kiislamu katika mizozo ya wenyewe kwa
wenyewe na kuongeza kuwa: Kama nchi kubwa za Kiislamu zitakuwa kitu
kimoja na kufikiria manufaa makuu ya Waislamu, basi itakuwa ni rahisi
sana kutatua matatizo yanayoyakumba mataifa ya Kiislamu.
Aidha amebainisha kuwa, baadhi ya nchi za Kiislamu badala ya
kushirikiana kiutamaduni na kiuchumi zenyewe kwa zenyewe, zinakimbilia
kwa mataifa ya nje ya eneo hili na kuongeza kuwa: Ni jambo la
kusikitisha kuona kuwa nchi fulani inachukizwa na ushindi wa taifa
fulani katika uga wa kisiasa na inapeleka rasilimali ya kisiasa ya
ulimwengu wa Kiislamu mikononi mwa madola ya kibeberu kwa thamani ya
chini kabisa.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameongeza kuwa: Nchi ambayo
imechangia pakubwa katika kuporomoka bei ya mafuta duniani, hivi sasa
imekumbwa na nakisi ya dola bilioni mia moja katika bajeti yake ijayo na
hili linaonesha kuwa mtu ambaye anawachimbia kisima watu wengine, yeye
mwenyewe huwa wa kwanza kutumbukia kwenye kisima hicho.
Mwishoni mwa mkutano huo, wageni kadhaa walioshiriki kwenye mkutano wa
29 wa Umoja wa Kiislamu wamepata fursa ya kuonana na kuzungumza kwa
karibu na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu.