Katika mahojiano na IQNA, Abu Bakr Mohammad Omar, ambaye ni hafidh wa Qur'ani Tukufu, amesema mashindano ya Qur'ani ya Iran huwaleta pamoja quraa, hufadh, na wataalamu wa Qur'ani Tukufu kutoka kila pembe ya dunia na hivyo kuandaa mazingira ya kuimarisha umoja wa Waislamu.
Ameongeza kuwa Qur'ani Tukufu ni kitabu kitukufu cha Waislamu na ni mhimili wa Umoja wa Ummah.
Aidha ameashiria harakati za Qur'ani nchini Tanzania, nchi ambayo ina Waislamu wengi zaidi Afrika Mashariki. Amesema katika nchi hiyo hufanyika mashindano ya kimataifa ya Qur'ani kila mwaka.
Kwingineko, Ustadh Rajayi Ayoub mwakilishi huyo wa Tanzania katika kitengo cha qiraa amesema washiriki wa mashindano ya kimatiafa ya Qur'ani ya Iran mwaka huu wameonyesha ustadi mzuri sana. Aidha amesema kiwango cha mashindano ni cha juu na ni mashindano yaliyoandaliwa vizuri sana.
Mashindano ya 33 ya Kimataifa ya Qur’ani Tukufu ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran yalizinduliwa rasmi Jumatano usiku katika Ukumbi Mkubwa wa Sala wa Imam Khomeini MA mjini Tehran.
Nchi zaidi ya 70 zimetuma wawakilishi katika Mashidano ya Kimataifa ya
Qur'ani hayo katika mji mkuu wa Jamhuri ya Kiislamu ya
Iran. Kuna washiriki 130 katika mashindano hayo ambayo kaulimbiu yake ni
"Kitabu Kimoja Umma Moja”.