IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Vyuo Vikuu, msingi wa kufikia malengo ya Jamhuri ya Kiislamu

16:37 - June 19, 2016
Habari ID: 3470398
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameainisha malengo ya mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu kwa ajili ya kuifanya Iran kuwa na nguvu, heshima na huru na kusema kuwa vyuo vikuu ni msingi mkuu wa kufanikisha malengo hayo.

Ayatullah Ali Khamenei alisema hayo jana jioni hapa mjini Tehran mbele ya wahadhiri wa vyuo vikuu, watafiti na watu wenye vipaji vya kielimu aliowaalika kwenye dhifa ya futari.

Amesema, kuongezwa kasi ya ukuaji wa kielimu katika vyuo vikuu na vituo vya kielimu, kuleta na kutia nguvu utambulisho wa kujivunia wa Kiirani - Kiislamu ndani ya nyoyo za vijana na kuhakikisha vyuo vikuu vinakuwa vya kimapinduzi pamoja na wanavyuo wake, ni katika mambo ya lazima ya kuufanya mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu kuwa nguvu kubwa ya kielimu duniani na pia kuwa kigezo kizuri cha mfumo wa demokrasia iliyosimama juu ya mafundisho ya Uislamu na umaanawi, ulimwenguni.

Amesema, vyuo vikuu nchini Iran vinapaswa kujipamba kwa sifa hizo na kulea vijana waumini na wenye itikadhi thabiti kama tunataka kulifanya taifa hili kuwa na mustakibali unaotakiwa wa Iran yenye nguvu, huru, iliyoshikamana na dini, tajiri, yenye uadilifu na yenye utawala wa wananchi, safi, yenye uchungu na dini, yenye watu wema na yenye kupigana jihadi katika nyuga zote. huku akichora na kubainisha malengo ya miaka 20 ya mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu kwa ajili ya kuifanya Iran kuwa yenye nguvu, yenye heshima, huru, iliyoshikamana na dini, tajiri, yenye uadilifu na utawala wa wananchi, safi, inayopigana jihadi, yenye uchungu na dini na ya watu wanaojiweka mbali na maasi, amesema kuwa, vyuo vikuu ni msingi mkuu wa kufanikishia malengo hayo na kusisitiza kuwa: Kuongeza kasi ya ustawi na ukuaji wa kielimu katika vyuo vikuu na vituo vya kielimu nchini, kuleta na kutia nguvu hisia za kujali utambulisho wa kujivunia wa Kiirani - Kiislamu kati ya vijana, vyuo vikuu kuwa vya kimapinduzi na wanafunzi wa vyuo hivyo nao kuwa wanamapinduzi pamoja na kutoa mchango wa kweli unaotakiwa wa makamanda na maafisa wa vita laini, ni miongoni mwa mambo ya lazima ya kuufanya mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu kuwa dola lenye nguvu kubwa ya kielimu na kigezo cha demokrasia iliyosimama juu ya msingi wa mafundisho ya Kiislamu na umaanawi duniani.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza katika mkutano huo juu ya wajibu wa kufanyika vikao zaidi kati yake na wahadhiri wa vyuo vikuu kwa lengo la kuonyesha heshima yake na kuenzi elimu na wahadhiri wa elimu nchini. Vile vile amegusia mambo mbali mbali yanayomuunganisha na watu wa vyuo vikuu, watu wenye vipaji vya kielimu na wanachuo na kuongeza kuwa: Kufanyika vikao vya namna hiyo mbali na uzuri wake wa dhahihiri, kunaonesha pia taswira jumla ya anga nzuri ya mijadala ya kielimu na kifikra ya vyuo vikuu.
Baada ya hapo Ayatullah Udhma Khamenei amesema kuwa, mtazamo kuhusu mustakbali wa nchi ni katika daghadagha na wasiwasi mkubwa wa weledi wa mambo, watu wenye hekima na watu wenye vipawa katika kila nchi. Ameongeza kuwa: Suala la kuchora malengo ya mustakbali lina umuhimu mkubwa kwani uongozi wa nchi katika miaka ijayo uko mikononi mwa wanafunzi wa vyuo vikuu ambao hivi sasa wako katika masomo wakifanya juhudi mbali mbali za kujiimarisha kielimu.
Amesema, suala hilo linaonesha ukubwa wa nafasi na hadhi ya wahadhiri na wakuu wa vyuo vikuu na kusisitiza kuwa: Kupewa umuhimu silisila ya elimu na maarifa, kuanzia Wizara ya Elimu na Malezi hadi vyuo vikuu ndilo jukumu kuu la kuwezesha kufikia mustakbali unaotakiwa na nchi.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameuliza swali kwamba, mustakbali unaotakiwa na Iran baada ya miaka 20 ni upi? Ameendelea kusema: Kama mustakbali unaotakiwa kwa ajili ya Iran ni kuwa na nchi yenye nguvu, yenye heshima, huru, iliyoshikamana na dini, tajiri, yenye uaduilifu, yenye utawala wa wananchi, safi, inayopigana jihadi, yenye uchungu wa dini na ya watu wanaojiweka mbali na maasi, basi kuna udharura kwa vyuo vikuu nchini kujipambana kwa sifa hizo na kulea kizazi cha vijana wenye itikadi za kidini na waumini wa kweli.
Ayatullah Udhma Khamenei amesisitiza kuwa: Kama vielelezo hivyo vitapewa kipaumbele katika vyuo vikuu, basi katika siku za usoni; Iran haitokuwa tegemezi katika upande wa kiutamaduni na itapata kinga mbele ya matatizo ya kijamii, kikaumu, kimadhehebu na kisiasa na pia itaepukana na utawala wa kibwanyenye na wa viongozi wapenda anasa na starehe.
Aidha amesema: Matunda ya mustakbali wa viongozi mabanyenye na wapenda anasa na starehe ni kuwa na nchi ambayo itakuwa katika vilele vya utajiri, lakini wakati huo huo itakuwa na watu maskini kupindukia, wenye shida na matatizo mengi ambapo mfano wa jamii kama hiyo ni jamii ya Marekani na mfumo wa Wall Street wa Kimarekani (wa uchumi uliohodhiwa na watu wachache huku idadi kubwa ya watu wakiwa hawana dhamana ya mustakbali mzuri katika maisha yao).
Kiongozi Mudhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa: Katika mustakbali wa nchi yenye viongozi wa aina hiyo, matabaka yote ya watu katika jamii yatashindwa kuwa na maisha mazuri na ustawi katika maisha yao, na wakati huo nchi yetu itakuwa na Wall Street ya Kiirani (ya mfumo wa kidhulma wa kiuchumi).
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ametoa muhtsari wa matamshi yake hadi kufikia hapo kwa kusema: Ni kwa sababu hii ndio maana mimi mara zote huwa ninasisitizia mno suala hilo kupewa umuhimu mkubwa vyuo vikuu, wahadhiri wa vyuo vikuu na wizara ya sayansi kwani ili kuweza kufikia kwenye mustakbali wa Iran inayotakiwa, kuna wajibu wa kulea watu wasomi, wenye subira, wanaopigana jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu, weledi wa mambo na mashujaa, ambapo sehemu kubwa ya watu wa namna hiyo hulelewa katika vyuo vikuu.
Ayatullah Udhma Khamenei ameendelea kubainisha mambo ya lazima ya kulea vijana wa namna hiyo katika vyuo vikuu na kusema: Maendeleo ya kielimu, nidhamu ya kimaadili, kuwa na subira na uvumilivu wa kidini, kuwa na busuri na muono wa mbali wa kisiasa na kuleta hisia za kuheshimu utambulisho wa Kiirani - Kiislamu na kujifakharisha nao katika vyuo vikuu, ni miongoni mwa mambo ya lazima ya jukumu hilo muhimu.
Amma kuhusiana na maendeleo ya kielimu, Ayatullah Udhma Khamenei amesisitizia ulazima wa kuongezwa kasi ya ustawi wa kielimu nchini na kuongeza kwa kusema: Hivi karibuni nilitoa ukumbusho kuhusu kupungua kasi ya ustawi wa kielimu, kwani kasi hiyo ni kweli imepungua na hakuna njia nyingine ya kuweza kufidia kubakishwa nyuma kielimu isipokuwa kuongeza kasi yetu ya ustawi wa kielimu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amegusia pia matamshi ya baadhi ya wanafikra kuhusiana na kupungua kasi ya ustawi wa kielimu katika nchi za Magharibi na kuongeza kuwa: Kama kasi ya ukuaji wa kielimu imepungua katika nchi za Magharibi sababu yake ni kuwa, nchi hizo tayari zimeshatumia sehemu kubwa ya uwezo wao wa kuhimili kasi hiyo, lakini sisi tuna wajibu wa kuziba pengo la kubakishwa nyuma kielimu kwa kipindi cha miaka sitini hadi sabini jambo ambalo limefanywa na tawala za wasaliti na zilizokuwa zimekumbwa na mghafala nchini (kabla ya ushindi Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran), ili kwa kuziba pengo hilo tuweze kujiweka kwenye nafasi ya juu na katika vilele vya juu katika mashindano haya ya kimataifa.
Ayatullah Udhma Khamenei amegusia pia nafasi ya wahadhiri wa vyuo vikuu katika kuleta na kutia nguvu utambulisho wa Kiirani na Kiislamu ndani ya wanafunzi wa vyuo vikuu na kusema kuwa: Wahadhiri wa vyuo vikuu wanapaswa kuwabainisha wanachuo maendeleo yaliyopigwa na nchi yao katika nyuga za anga za mbali, teknolojia za Nano na nyuklia pamoja na teknolojia za masuala ya kibiolojia ya kimatibabu, ili kwa njia hiyo tuweze kuwajengea wanachuo hao utambulisho wa kujivunia wa Kiirani na Kiislamu.
Vile vile amesisitiza kuwa, hatua yoyote ile ya kuleta hisia za kujiona duni na kuwavunja moyo wanachuo ni usaliti na kuongeza kwamba: Wanafunzi wa vyuo vikuu wanapaswa wakati wote kujivunia na kuona fakhari kuwa kwao Wairani, Waislamu na wanamapinduzi.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza pia kwamba: Ijapokuwa sisi tumebakishwa nyuma kihistoria katika maendeleo ya kielimu, lakini kwa jitihada na jitihada kubwa za vijana wetu wenye vipawa vya kila aina nchini, tunaweza kufidia na kuziba pengo hilo bila ya wasiwasi wowote ule.
Ayatullah Udhma Khamenei ameashiria pia ripoti za baadhi ya taasisi za nyaraka na takwimu pamoja na majarida yenye itibari duniani yaliyothibitisha kupigwa hatua kubwa za maendeleo ya kielimu nchini Iran na kuongeza kuwa: Katika ripoti hizo, taasisi na majarida hayo maarufu na yenye itibari duniani yanapozungumzia maendeleo mbali mbali ya kielimu ya Iran huwa yanatumia maneno kama "maendeleo ya kustaajabisha ya Iran," "Iran dola linalochipua lenye nguvu za kielimu," "Iran katika juhudi za kubadilisha uchumi unaotegemea maliasili kuwa uchumi unaotegemea uzalishaji wa elimu" na "maendeleo ya Iran katika seli shina, sayansi ya teknolojia, anga za mbali, kubadilisha nishati na teknolojia ya mawasiliano." Amesema, inabidi uhakika huo ufikishwe vizuri kwa kizazi cha vijana nchini ili sambamba na kupata hisia za kupenda utambulisho wao, waweze kujivunia na kuona fakhari kuwa kwao Wairani.
Amesema, ubunifu mpya uliokuja nao mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran duniani katika nyuga za demokrasia ni kitu kingine muhimu cha kujivunia na kusisitiza kwamba: Mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ndio utawala pekee duniani ambao umekuja na demokrasia iliyosimama kwenye msingi wa Uislamu na umaanawi.
Kiongozi Mudhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa: Demokrasia ya nchi za Magharibi kwa hakika ni utawala wa vyama, na vyama katika nchi za Magharibi badala ya kuwa kanali iliyojitanua na yenye uungaji mkono wa wananchi, kimsingi ni klabu za kisiasa ambazo zimezoundwa na baadhi ya wanasiasa na mabepari, bila ya kujali nafasi ya wananchi na maamuzi yao.
Ayatullah Udhma Khamenei amekumbusha pia kuwa: Kama uhakika huo wa kujivunia utafikishwa vizuri kwa mwanafunzi wa chuo kikuu, mwanafunzi huyo hatoweza kujiona duni wala kukata tamaa, na hata kama atakwenda nje ya nchi kwa ajili ya kuendelea na masomo, bila ya shaka yoyote atarejea nchini kwake kwani atakuwa tayari amejengeka vizuri kwa hisia za kujali utambulisho wake na kujifakharisha nao.
Aidha amesema kuhusiana na kupewa kipaumbele utambulisho wa Kiislamu katika vyuo vikuu nchini kuwa: Viongozi wa vyuo vikuu wana wajibu wa kusimama imara kukabiliana na pia kuzuia hatua au jambo lolote lile lisilokubaliwa na Uislamu kama vile kupigwa kambi tofauti za wanachuo ambazo zinatia doa utambulisho wa Kiislamu.
Kuwa na busuri na muono wa mbali wa kisiasa na kupewa nafasi kazi za kisiasa katika vyuo vikuu ni jambo jingine la lazima la kuweza kuwa na Iran yenye mustakbali unaotakiwa jambo ambalo limezungumziwa na Kiongozi Muadhamu katika matamshi yake hayo na kuongeza kwa kusema: Mimi nimekuwa nikisisitizia mara zote umuhimu wa kujadiliwa masuala ya siasa ndani ya vyuo vikuu na hata katika miaka ya huko nyuma niliwahi kusema kuwa, Mungu awalaani watu ambao walipiga marufuku upanuzi wa fikra na kufanyika kazi za kisiasa kwenye vyuo vikuu.
Ayatullah Udhma Khamenei ameongeza kwamba: Wakuu wa wakati huo walikasirishwa sana na maneno yangu hayo, lakini itikadi ya viongozi hao ilikuwa ni kupigwa marufuku na kuzuiwa masuala ya siasa ndani ya vyuo vikuu ingawa leo hii watu hao hao wanajitoa kimasomaso na kutoa matamshi tofauti na itikadi zao za huko nyuma kuhusiana na vyuo vikuu.
Vile vile amesisitiza kuwa, anga ya vyuo vikuu ni anga ya kuchuanisha mitazamo, mijadala na kutoa changamoto za kila namna na kuongeza kuwa: Kuweko anga hiyo katika kipindi ambacho damu za wanachuo vijana zinachemka mwili, hakuna tatizo lolote, tatizo linakuja pale anga hiyo inapotumika kwa ajili ya kupiga vita Mapinduzi ya Kiislamu na kutumiwa vibaya kukabiliana na matukufu ya Mapinduzi ya Kiislamu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa: Hakuna tatizo kuweko mitazamo na mirengo tofauti ya kisiasa katika vyuo vikuu, lakini maafisa na viongozi wa vyuo hivyo - iwe ni viongozi wa ngazi za juu au wizara au marais au wahadhiri - kila mmoja ana jukumu la kuielekeza anga hiyo ya michuanisho ya hoja katika vyuo vikuu, upande wa kutia nguvu misingi na malengo ya Mapinduzi ya Kiislamu na kamwe wasiruhusu kuweko mitazamo ya kupinga Mapinduzi ya Kiislamu katika vyuo vikuu.
Ayatullah Udhma Khamenei aidha amesisitiza kuwa: Vyuo vikuu na wanachuo, wanapaswa kuwa wanapinduzi daima.
Vile vile ameashiria baadhi ya ripoti zinazoonesha kuweko fikra za kuunga mkono mirengo inayopinga mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu katika baadhi ya vyuo vikuu na kuongeza kuwa: Wakuu wa Wizara ya Sayansi na Elimu ya Juu wanapaswa kuwa macho sana, na wasiruhusu vyuo vikuu kugeuzwa kuwa maeneo ya kupotosha na kupiga vita uhakika na matukufu ya Mapinduzi ya Kiislamu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza pia kuwa: Kuweko anga ya kimapinduzi na ya kushikamana na dini na kupewa nafasi kubwa Imam (Khomeini - Rahimahullah) kwenye vyuo hivyo, ni katika mambo ya lazima ya wazi kabisa kwa vyuo vikuu.
Ayatullah Udhma Khamenei ameendelea na hotuba yake kwa kusema: Tab'an si sahihi pia kuleta anga ya kulazimisha na kutenza nguvu katika vyuo vikuu, lakini anga ya vyuo hivyo inapaswa kuwa ya kimapinduzi na kidini, na hilo linapaswa kufanikishwa kwa hekima, kwa utulivu na kwa busra ya hali ya juu.
Kiongozi Mudhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameendelea na hotuba yake kwa kutoa nasaha kadhaa kwa maafisa na wakuu wa Wizara ya Sayansi na Elimu ya Juu pamoja na wakuu wa vyuo vikuu nchini.
Kulindwa na kuhifadhiwa moyo wa matumaini na nishati na uchangamfu katika maeneo ya kielimu na kiutafiti, kuzipa kipaumbele na umuhimu elimu za kimsingi, kuelekeza makala za kielimu upande wa mahitaji ya nchi, ulazima wa kubainishwa na kutolewa ufafanuzi ramani kuu ya kielimu nchini kwa ajili ya watu wa vyuo vikuu na kuifanya ramani hiyo kuwa ajenda yao na kutiliwa mkazo umuhimu wa kuweko masomo ya Sayansi ya Jamii yaliyosimama kwenye msingi wa dini tukufu ya Kiislamu, ni katika nasaha zilizotolewa na Ayatullah Udhma Sayyid Ali Khamenei kwenye hotuba yake hiyo.
Kupewa umuhimu udiplomasia ya kielimu ni nasaha nyingine zilizotolewa na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika hotuba yake hiyo ambaye wakati huo huo amesisitiza kwa kusema: Udiplomasia na uhusiano wa kielimu ni jambo muhimu, nami ninaliunga mkono jambo hilo, lakini inabidi tuwe macho tusije tukatekwa na hila za maadui na kugeuzwa uhusiano huo wa kielimu kuwa bwawa la kujipenyeza na kutia doa maadui katika masuala yetu ya usalama kwani adui anatumia kila njia ikiwa ni pamoja na uhusiano na mawasiliano ya kielimu kwa ajili ya kujipenyeza nchini na kwamba jambo hilo limewahi kutokea huko nyuma na madhara yake yanaonekana leo hii katika baadhi ya mambo.
Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Ayatullah Udhma Khamenei amezungumzia uchumi wa kimuqawama na kusema kuwa uchumi huo utaandaa uwanja wa kupatikana heshima ya kitaifa na kutatua matatizo yote yaliyopo hivi sasa nchini. Ameongeza kuwa: Kuna baadhi ya watu wanasema, vipi utaweza kutatua matatizo na shida za hivi sasa katika jamii kupitia kusisitizia mara kwa mara suala la kulindwa heshima ya taifa? Majibu ya watu wanaotoa maneno hayo ni kwamba: Utatuzi pekee wa jambo hilo ni kutekelezwa vilivyo na kwa njia sahihi siasa za uchumi wa kimuqawama.
Nasaha nyingine zilizotolewa na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ni umuhimu na kuyafanya kuwa jambo la kimsingi masuala ya kiutamaduni kwenye vyuo vikuu.
Ameongeza kwa kusema: Tab'an masuala ya kiutamaduni hayana maana ya kufanya mambo madogo madogo ya pembeni au kupeleka wanafunzi kwenye kumbi za muziki na tamthilia, bali viongozi wa vyuo vikuu wanapaswa kuwafunguliwa uwanja wanachuo na wahadhiri wa vyuo hivyo wanaojali mambo ya thamani na ya maana, ili waweze kufanya kazi zao vizuri kwa ajili ya kuzijaza akili na nyoyo za wanafunzi wa vyuo vikuu, utamaduni wa Kiislamu na wa kimapinduzi.
Ayatullah Udhma Khamenei vile vile amewalenga moja kwa moja katika maneno yake wahadhiri wanamapinduzi ambao ni makamanda katika vita laini pamoja na wanachuo wanamapinduzi ambao ni maafisa katika vita hivyo laini akiwasisitizia kwa kuwaambia: Jukumu lenu ni kutoa mchango wa kweli na unaotakiwa katika shauri hili kwani ugumu na ukali wa vita laini vinavyoendeshwa na adui hivi sasa ni mkubwa zaidi kwa mara kadhaa ikilinganishwa na miaka ya huko nyuma.
Kutoruhusu kujiingiza na kutumiwa watu wasioaminika katika vyuo vikuu, ni nasaha nyingine zilizotolewa na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ambaye amesisitiza kuwa: Mtu yeyote ambaye atatumia kisingizio chochote kile kama vile uchaguzi na mfano wake ili kuutia kwenye matatizo mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu, mtu huyo haaminiki, na hana sifa za kuweko katika vyuo vikuu, na hilo si jambo jipya kwani hakuna nchi yoyote duniani inayoruhusu mfumo wake wa utawala utiwe katika matatizo.
Mwanzoni mwa mkutano huo, baadhi ya wahadhiri, wanafikra na wataalamu wa fani za sayansi ya uhandisi, sayansi ya tiba na sayansi ya jamii wametoa hotuba fupi fupi na kubainisha mitazamo yao kuhusiana na masuala tofauti.

3508195

captcha