Ayatullah Ali Khamenei amesema hayo leo mjini Tehran alipokutana na hadhara kubwa ya matabaka mbalimbali ya wananchi kwa mnasaba wa Sikukuu ya Ghadir Khum ambapo sambamba na kutoa mkono wa kheri, baraka na fanaka kwa Waislamu wote ulimwenguni kwa mnasaba wa maadhimisho hayo amesema kuwa, ujumbe muhimu kabisa wa Ghadir ulikuwa ni kuainisha suala la Uimamu ukiwa kama ni kanuni ya utawala katika Uislamu. Ayatullah Khamenei amebainisha kwamba, tukio la Ghadir lilikuwa ni kuwekwa jiwe la msingi la utawala katika jamii ya Kiislamu na hilo linaonyesha kuwa, ghairi ya utawala wa Uimamu na Wilaya, Uislamu haukubaliani na aina nyingine za utawala kama, utawala wa kifalme, wa kibinafsi, wa utumiaji mabavu, wa kutaka makuu, wa ujeuri, wa kufuata matamanio ya nafsi na wa kibwanyenye.
Ayatullah Khamenei ameashiria sifa za kipekee za Amirul-Muumina Ali bin Abi Twalib AS hususan sifa za utawala wake ukiwemo uadilifu, insafu, kuiongoza jamii kuelekea katika uchaji Mungu na kujiepusha na mambo ya kipuuzi na kusisitiza kwamba, kuwa na imani imara, kutangulia katika Uislamu, ikhlasi na kujitolea katika njia ya Uislamu ni miongoni mwa sifa za kimaanawi na za kiutu za Imam Ali bi Abi Twalib AS.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa,
lengo kuu la adui kwa sasa ni kukwamisha uchumi wa Iran ili kuleta hali
ya kutoridhika miongoni mwa wananchi. Aidha Ayatullah Khamenei amesema
kuwa, katika mazingira ya hivi sasa jukumu la serikali, Bunge na
maafisa wengine katika sekta mbalimbali na vilevile wananchi ni kuandaa
mipango na kuchukua hatua ambazo zitakabiliana na malengo ya adui.Sambamba na maadhimisho ya sikukuu ya Ghadir, idi ya Uimamu na Wilaya,
na sikukuu ya Allahu Akbar, leo asubuhi (Jumanne), Kiongozi Muadhamu wa
Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Udhma Sayyid Ali Khamenei ameonana na
maelfu ya wananchi wa matabaka tofauti katika Husainia ya Imam Khomeini
(quddisa sirruh) mjini Tehran.
Katika mkutano huo, Kiongozi Muadhamu
wa Mapinduzi ya Kiislamu ametoa mkono wa baraka kwa mnasaba wa sikukuu
ya Ghadir na kusema kuwa, ujumbe muhimu zaidi unaopatikana katika tukio
la Ghadir ni kuainishwa Uimamu kuwa ndio msingi na kielelelezo cha
utawala katika Uislamu. Aidha amegusia sifa za kipekee za Imam Ali
(Alayhis Salaam) hususan namna alivyokuwa ametimiza sifa zote za
kuongoza dola ya Kiislamu, na amewausia hadhirina kuhusu ulazima wa
kushikamana na Wilaya na utawala wa Amirul Muminin, Imam Ali (Alayhis
Salaam) kupitia kutekeleza vizuri miongozo na nasaha za shakhsia huyo
mkubwa na wa aina yake.
Vile vile amegusia baadhi ya maneno
yanayotumika kuitambulisha sikukuu ya Ghadir kama vile kuiita idi kubwa
ya Mwenyezi Mungu na kusema kuwa, sababu ya kuweko majina hayo, ni tukio
muhimu sana ambalo lilitokea katika Ghadir, nalo ni kuainishwa kigezo
na kielelezo cha utawala ndani ya dola ya Kiislamu.
Ameongeza kuwa:
Kielelezo na kigezo hicho ni Uimamu na Wilaya katika jamii ya Kiislamu
na ambayo ni amri kutoka kwa Mwenyezi Mungu iliyotangazwa na Bwana Mtume
Muhammad SAW.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza
kuwa: Mbali na kuainisha kigezo na kielelezo, Imam Ali (Alayhis Salaam)
alitangazwa rasmi kuwa ni Imam akiwa ni shakhsia mkubwa, mtukufu,
aliyejaa nuru na ambaye si rahisi kumtia doa.
Ameongeza kuwa: Tab'an,
hakuna mtu yeyote aliyeweza kufikia kilele alichofikia Imam Ali AS
katika upande wa Uimamu na kuongoza jamii ya Kiislamu baada ya Bwana
Mtume SAW. Shakhsia wengine wakubwa wa kielimu na uchaji Mungu wamekuja
katika historia ya Uislamu, kama vile Imam wetu mtukufu (Imam Khomeini -
quddisa sirruh), lakini wote hao ni tone tu mbele ya miale iliyojaa
nuru ya Amirul Muminin Imam Ali (Alayhis Salaam).
Baada ya hapo
ametoa muhtasari wa maelezo yake hadi kufikia hapo kwa kusema: Tukio la
Ghadir liliweka msingi wa kigezo na kielelezo cha utawala katika jamii
ya Kiislamu na kusisitiza kwa kusema: Ukitoa kigezo cha Uimamu na
Wilaya, Uislamu haukubaliani na tawala nyinginezo zozote, za kisultani,
za watu binafsi, za kibeberu, za watu wanaopenda kujikumbizia kila kitu
upande wao, za watu wenye viburi na za watu wanaofuata matamanio ya
nafsi, anasa na ubwanyenye.
Vile vile amebainisha umuhimu wa kadhia
ya Ghadir ambayo Mwenyezi Mungu alimwamrisha Mtume Wake aitangaze na
kwamba risala aliyetumwa kuifikisha hatakuwa ameifikisha kama hakutanga
Uimamu na kuongeza kuwa: Itikadi hiyo ya Kiislamu imesimama juu ya
msingi madhubuti wenye hoja zisizokanushika, lakini pamoja na hayo,
wakati wa kuibainisha na kuitangaza itikadi hiyo, inabidi watu wawe
macho, wasije wakaitumia kujeruhi hisia za Waislamu wa Kisuni, kwani
kufanya hivyo ni kinyume na sira ya Maimamu maasumu (Alayhimus Salaam).
Kiongozi
Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza tena na tena kuhusu
umuhimu wa umoja na mshikamano katika ulimwengu wa Kiislamu na huku
akigusia kwamba, kusema maneno yoyote yale mabaya dhidi ya shakhsia
wakubwa na viongozi kwa Waislamu wa madhehebu mengine, kwa hakika ni
kuzuia kufika misingi ya kimantiki na yenye hoja madhubuti ya Uimamu.
Amesisitiza kuwa, kitendo chochote kile cha kuchochea hisia za watu wa
madhehebu mengine ya Kiislamu kwa jina la Ushia, kwa hakika huo si Ushia
halisi, bali huo ni Ushia wa Kiingereza na matokeo yake ni kujitokeza
magenge khabithi na mamluki wa Marekani na wa shirika la kijasusi la
Uingereza kama vile Daesh na Jabhatun Nusra ambayo yanafanya jinai na
kusababisha hasara kubwa kwa ulimwengu wa Kiislamu.
Ayatullah Udhma
Khamenei ameendelea na hotuba yake kwa kuashiria sifa za kimaanawi na
kiutu za Imam Ali AS kama vile kuwa na imani kubwa sana, kuwa wa mwanzo
kuingia katika Uislamu, kujitolea kikamilifu katika njia ya Uislamu,
ikhlasi, elimu, maarifa ya Allah, ushujaa, huruma, kujitolea na kusamehe
na kuongeza kuwa: Sehemu nyingine ya sifa za aina yake za mtukufu huyo
inahusiana na mbinu alizotumia katika kuongoza dola ya Kiislamu.
Miongoni mwa sifa hizo ni uadilifu, insafu na kuwaweka daraja sawa
wananchi wote, kujiweka mbali na anasa za kidunia, tadibiri,
kutochelewesha hata kidogo kutekeleza majukumu, uwazi, kuiongoza jamii
kuelekea kwenye taqwa na kufanya haraka sana katika kutenda haki na
uadilifu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema
kuhusiana na namna Imam Ali (Alayis Salaam) alivyojiepusha na anasa za
dunia au kutumia utawala katika mambo yake binafsi na kusisitiza kwamba:
Wasiwasi na ushawishi unaomkumba mtu, wa kutumia vibaya vyanzo vya
fedha vilivyo mikononi mwake kujinufaisha binafsi, ni miongoni mwa
mabalaa ambayo yanazitesa tawala zisizo za Mwenyezi Mungu, lakini
utawala ambao kigezo na kielelezo chake ni Uimamu na Wilaya, unapinga
vikali mambo kama hayo na unapiga marufuku kutumia mali ya umma kwa
mambo ya watu binafsi.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu
aidha amesema: Imam Ali (Alayhis Salaam) alikuwa akifanya tadibiri sana
katika kumjua rafiki na adui na katika kuwaainisha maadui na hayo
yanaonekana wazi katika hatua zilizochukuliwa na mtukufu huyo kwenye
vita vitatu alivyopigana na maadui baada ya kuwa kiongozi wa dola ya
Kiislamu. Hatua hizo zinatofautiana kulingana na mazingira ya kila vita.
Amesema,
Amirul Muminin Imam Ali (Alayhis Salaam) alikuwa ni shakhsia
aliyekusanya sifa za kila upande, alikuwa shakhsia adhimu na ambaye ni
vigumu kuzungumzia ipasavyo wasifu wake. Amesema, jukumu letu sisi ni
kujitahidi kupiga hatua kuelekea kwenye kilele hicho na kustafidi
ipasavyo na sifa zake hizo kwa kadiri ya uwezo na kiwango cha imani
yetu.
Ayatullah Udhma Khamenei amegusia pia ulazima wa kujipamba
Mashia kwa tabia na maadili ya Ahlul Bait AS na kusema: Mtu ambaye
anapokea rushwa au anatumia "Baitul Maal" kwa manufaa yake binafsi au
anayekodolea macho maovu na ambaye hana hisia zozote mbele ya wajibu wa
kuiongoza vizuri jamii, mtu huyo si fakhari wala si pambo kwa Jamhuri ya
Kiislamu wala kwa jamii ya Kiislamu, bali ni aibu kwa Mashia.
Kiongozi
Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu pia amesema, sisi kamwe hatuwezi
kuishi kama alivyokuwa akiishi Imam Ali (Alayhis Salaam) kwa uchaji
mkubwa mno wa Mwenyezi Mungu, lakini pamoja na hayo tunaweza kuingia
kwenye mkondo wa njia hiyo iliyojaa nuru kwa kujiweka mbali na israfu na
kuchupa mipaka. Aidha amesema: Inasikitisha kuona kuwa, jamii yetu
imekumbwa na jambo la aibu la israfu na israfu nayo iko kwa sura nyingi
miongoni mwake ni israfu katika maisha binafsi ya mtu.
Ayatullah
Udhma Khamenei amesema, moja ya madhara ya israfu katika jamii, ni
kuharibu uchumi wa nchi. Ameongeza kuwa: Kama jamii inataka kuwa na
nguvu za ndani za kiuchumi na kufikia daraja ya juu inayotakiwa, basi
jamii hiyo haina njia nyingine ila kupambana na israfu.
Kiongozi
Mudhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema, jukumu la kwanza kabisa la
wananchi ni kupambana na israfu na huku akisisitiza kuwa kushikamana na
Wilaya na Uimamu wa Imam Ali AS inabidi kuonekane kivitendo amesema:
Moja ya njia zinazotumiwa na adui kutoa pigo, ni kutumia udhaifu wa
jamii, hivyo kuna wajibu wa kurekebishwa udhaifu wowote unaojitokeza.
Ayatullah
Udhma Khamenei aidha amesema, lengo kuu la adui hivi sasa ni kuvuruga
uchumi wa Iran na huku akigusia namna ambavyo amekuwa akisisitizia mara
kwa mara suala la kushikamana na uchumi wa kimuqawama amesema:
Anachopigania adui ni kuharibu uchumi wa wananchi ili hatimaye wananchi
hao wauchukuie Uislamu na mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu.
Amesisitiza
kuwa: Kwa kuzingatia hali hiyo, ni jukumu la Serikali, Bunge na maafisa
wa sekta nyingine za wananchi kuwa na mipango mizuri ya kukabiliana na
njama hizo za adui.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu
amemshukuru Mwenyezi Mungu kutokana na harakati nzuri za vijana wa Iran
katika kuuhuisha Uislamu na kusimamisha dini na kusema, vijana hao kwa
uwezo wa Mwenyezi Mungu watampigisha magoti adui yeyote yule ikiwemo
Marekani na utawala wa Kizayuni.
Ayatullah Udhma Khamenei
amesisitiza kuwa: Sababu inayonifanya nisisitize mno katika maneno yangu
kwamba nina mtazamo mzuri na matumaini ya mustakbali mwema ni kuweko
vijana kama hawa na uhakika kama huu ambao unao uwezo wa kuifanya nchi
isonge mbele.
Vile vile amesema, vijana walio imara kiimani, wenye
msukumo wa hali ya juu na walio tayari wakati wote kuingia katika medani
za jihadi na kulinda nchi, ni wengi nchini Iran. Amesisitiza kuwa: Huu
ndio huo msukumo ambao utaweza kuiokoa nchi, hivyo kuna wajibu wa
kuuimarisha na kuutia nguvu msukumo huo.