Ayatullah Seyyed Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameyasema hayo leo haoa mjini Tehran alipokutana na wasomi bingwa waliopata medali za olimpiadi za kisayansi kutoka Chuo Kikuu cha Teknolojia cha Shariff na kuongeza kuwa, sababu ya kuwepo nyufa, mapungufu na kulegalega katika misingi ya ustaarabu wa Magharibi ni kuwepo ustawi mkubwa wa kimaada pasina kuwepo umaanawi na mafundisho ya Mwenyezi Mungu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa, baadhi ya wasomi na wanafikra wa Marekani wamekiri wazi wazi kuwepo upotovu mwingi wa kifikra, kimaadili, kusambaratika misingi ya failia, kuongezeka utumiaji wa mabavu, ufisadi wa kimaadili, vitendo vya kujiua katika jamii za Magharibi hasa Marekani.
Kiongozi Muadhamu ameashiria kuongezeka vitendo vya utumiaji mabavu nchini Marekani na mauaji ya kutumia silaha na kusema, mauaji na kuenea silaha mikononi mwa wananchi ni tatizo kubwa la Marekani. Amesema njia ya kukomesha tatizo hilo ni kusitisha utumiaji wa silaha miongoni mwa wananchi lakini kutokana na satwa ya kimafia ya mashirika yanayotengeneza silaha nchini Marekani, watawala wa nchi hiyo hawathubutu kupiga marufuku utumiaji silaha kiholela nchini humo.
Kwingineko katika matamshi yake, Ayatullah Khamenei amesema ufanikishaji wa uchumi wa kimapambano au kimuqawama ni jambo linalotegemea malengo ya nchi na kuongeza kuwa, ni jambo linalokubalika kuwa, uchumi wa kimuqawama nchini Iran utaweza kuilinda nchi na kuiwezesha kukabiliana na mibinyo na mashinikizo mbalimbali duniani iwe ni kutoka kwa wasioitakia mema au hata wanaoitakia mema nchi hii.
Aidha Kiongozi Muadhamu ameashiria sababu ya kustawi Marekani kisayansi na kiviwanda katika miaka 150 iliyopita na kusema, Marekani imekiwa ikitumia uchumi wa kimapambano na kusema kuwa, tab'an Marekani imekuwa ikitumia fikra hiyo kwa ajili ya malengo la kimaada na kujirundikia utajiri. Ameongeza kuwa, uchumi wa kimuqawama ni uzoefu uliokubalika duniani na unaweza kutumiwa kwa ajili ya ustawi wa nchi.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu halikadhalika amesisitiza kuwa, kuenea fikra ya kuzalisha elimu na kutekeleza kivitendo, pamoja na jitihada na harakati za kielimu Iran hazipaswi kusimamishwa bali zinapaswa kuchukua mwendo wa kasi zaidi.
3558832