IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Wamagharibi wanataka kudhibiti eneo kupitia vita dhidi ya Uislamu

22:32 - May 01, 2016
Habari ID: 3470283
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema madola ya Magharibi yakiongozwa na Marekani yanataka kulidhibiti eneo la Magharibi mwa Asia kupitia vita vikubwa na vipana dhidi ya mrengo wa Uislamu.
Ayatullah Seyyed Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameyasema hayo leo alasiri mjini Tehran alipokutana na kufanya mazungumzo na Ramadhan Abdullah, Kiongozi wa Harakati ya Jihad Islami ya Palestina. Akitoa tathmini jumla kuhusu hali ya hivi sasa katika eneo amesisitiza kuwa: "Vita vipana vinaendelea sasa katika eneo. Vita hivi ni muendelezo wa vita vya miaka 37 iliyopita ambavyo vilianzisha dhidi ya Iran."
Kiongozi Muadhamu amesisitiza kuwa, msimamo wa Iran kuhusu Palestina si msimamo wa kipindi fulani tu na kuongeza kuwa: "Kabla ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu na katika zama za mapambano, msimamo wa kuunga mkono Palestina na kukabiliana na utawala wa Kizayuni ulikuwa msimamo wa mara kwa mara wa Imam Khomeini MA na baada ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu vile vile, kuunga mkono watu wa Palestina kulikuwa moja kati ya hatua za awali za Iran. Kwa hivyo kuunga mkono malengo matukufu ya Wapalestina, ni jambo ambalo liko katika dhati ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran."
Ayatullah Khamenei ameashiria mashinikizo mbali mbali na mapana ya kisiasa, kipropaganda ,kiuchumi na hata ya kijeshi ili kupigisha magoti Mapinduzi ya Kiislamu au kuufanya mfumo wa Kiislamu uachane na misimamo yake. Ameongeza kuwa, kile ambacho kinajiri leo katika eneo ni muendelezo wa makabiliano ya Marekani na Mfumo wa Kiislamu wa Iran.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema lengo kuu la vita vipana vya sasa vya mrengo wa Magharibi ukiongozwa na Marekani dhidi ya mrengo wa Kiislamu ni kulidhibiti eneo la Magharibi mwa Asia. Amesema matukio ya eneo hili yanapaswa kutathminiwa kwa mtazamo huu; na kwa msingi huo, masuala ya Syria, Iraq, Lebanon, na Hizbullah ni kati ya makabiliano haya.
Ayatullah Khamenei amesisitiza kuwa, katika hali kama hii, 'kutetea Palestina ni nembo ya kutetea Uislamu"
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ameongeza kuwa, mrengo wa madola ya kibeberu na kiistikbari yametekeleza jitihada kubwa kwa ajili ya kuarifisha makabiliano ya sasa katika eneo kuwa eti ni 'vita baina ya Shia na Suni.
Ayatullah Khamenei amebaini kuwa, "nchini Syria serikali si ya Kishia , lakini Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inaunga mkono serikali ya Syria. Hii ni kwa sababu watu wanaokabiliana na Syria ni maadui wa Uislamu na wanahudumia maslahi ya Marekani na utawala wa Kizayuni."
Ayatullah Khamenei aidha ameashiria matamshi ya Katibu Mkuu wa Jihad Islami kuhusu baadhi ya njama za kuishinikiza harakati ya Hizbullah ya Lebanon na kusema: "Hizbullah ya Lebanon ina nguvu zaidi na haiwezi kuathiriwa na hatua dhidi yake. Leo bila shaka utawala wa Kizayuni unaiogopa Hizbullah zaidi."
3493905
captcha