Hujjatul Islam Sayyed Mustafa Husseini Mkuu wa Masuala ya Qur’ani katika Shirika la Awqaf la Iran ambalo linaandaa mashindano hayo ya Qur’ani amemwambia mwandishi wa IQNA kuwa, hadi sasa washiriki 283 wameshathibitisha kushiriki katika mashindano matano mbali mbali ya kimataifa ya Qur’ani nchini Iran mwaka huu.
Amesema mashindano hayo ni pamoja na Mashindano ya 34 ya Kimataifa ya Qur’ani Tukufu, mashindano ya kimataifa ya Qur’ani ya wanawake, mashindano ya kimataifa ya Qur’ani ya wanachuo vya vyuo vikuu vya kidini, mashindano ya kimataifa ya Qur’ani ya wenye ulemavu wa macho na mashindano ya kimataifa ya Qur’ani ya wanafunzi wa shule.
Hujjatul Islam Husseini amesema kwa kuzingatia watakaoandamana na washiriki pamoja na wageni waalikwa, kwa ujumla wageni wa nchi za kigeni watakaoshiriki katika mashindano hayo nchini Iran wanatazamiwa kufika 400.
Aidha amesema katika mashindano hayo matano, jopo la majaji litajumuisha wataalamu Wairani na kutoka nchi za kigeni na kwamba watatangazwa katika siku zijazo. Halikadhalika amesema mashindano hayo yote matano ya kimataifa yatafanyika nchini Iran mwezi Mei. Mwaka jana wasomaji na waliohifadhi Qur’ani kutoka nchi 70 walishiriki katika Mashindano ya Kimataifa ya Qur’ani nchini Iran.